Sunday, April 22, 2012

Tanesco taabani

BUNGE limeelezwa kuwa hali mbaya inayolikabili Shirika la Umeme (Tanesco) imefanya shirika hilo kusimamisha huduma yake ya kuwaunganishia wateja wapya umeme.

Lengo la Serikali ni kufikia walau asilimia 30 ya kaya za Watanzania wanaotumia umeme
ifikapo mwaka 2015 na ili kufikia lengo hilo, ilikadiriwa kuwa ni lazima Tanesco iunganishe wateja wapatao 137,000 kwa mwezi kuanzia Machi 2012.

“Kutokana na hali mbaya ya kifedha na kiuendeshaji wa shirika, lengo hili halitaweza kufikiwa
kwani Tanesco inashindwa kulipia vifaa vya kutosha kwa wakati,” alisema Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, January Makamba.

Alisema shirika kwa sasa linaelemewa na mzigo mkubwa na hali hiyo ikiendelea, litashindwa
kutimiza majukumu yake na akataka hali hiyo irekebishwe haraka kwani ipo hatari nchi kuingia
kwenye mgawo mkubwa wa umeme wakati wowote wa kiangazi.

Alisema pia kuwa kutokana na shirika hilo kuwa katika hali mbaya ya kifedha, wagavi wake wanatishia kusimamisha huduma mbalimbali kwa shirika hilo.

Pia Tanesco imeshindwa kupata fedha za kukarabati miundombinu ya usafirishaji na usambazaji wa umeme hali inayofanya kuongezeka kwa uhaba wa umeme.

Bunge pia liliambiwa na mwenyekiti huyo kuwa mpango wa dharura ulioahidiwa na Serikali
haujatekelezwa kwa kiasi na kiwango kama ilivyoahidiwa bungeni mwaka jana.

Makamba alisema katika megawati 572 zilizoahidiwa kuzalishwa kati ya Agosti 2011 hadi Desemba 2011 ni megawati 342 tu ndizo zimezalishwa.

Kutokana na hatari hiyo ya nchi kuingia gizani wakati wowote, Kamati hiyo ya Bunge imeishauri Serikali kutoa dhamana yake ili shirika hilo liweze kukopa fedha kiasi cha Sh bilioni 408 ili ilipie madeni yake.

Kwa upande wake, Kamati ya Fedha na Uchumi katika taarifa yake ilisema Tanesco inadaiwa Sh bilioni 105 na kampuni za kufua umeme wa dharura na Sh bilioni 164 zinadaiwa na wadeni wengine; hivyo kufanya hadi kufikia Machi mwaka huu, shirika hilo lilikuwa linadaiwa jumla ya Sh bilioni 269.

Lakini pia kamati hiyo imeonya kuwa kiasi cha Sh bilioni 408 zitakazochukuliwa na shirika hilo kama mkopo kutoka benki za ndani, gharama kubwa ya mkopo huo pamoja na ulipaji wa riba utafanya gharama za uzalishaji kuwa za juu kwa matumizi ya Tanzania.

“Malipo haya yanaongeza matumizi ya Serikali yenye ukusanyaji mdogo wa mapato,” alisema
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Fedha na Uchumi, Dk. Abdallah Kigoda.

Dk. Kigoda alisema mpango wa Serikali wa kuongeza umeme hautaleta tija ikiwa Gridi ya Taifa itaendelea kama ilivyo sasa.

Kwa upande wake, Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Mashirika ya Umma ni moja ya shirika linalotumia fedha za umma vibaya kinyume cha Sheria ya Manunuzi ya Umma.

Kamati hiyo imetoa mfano wa Tanesco kutumia Sh bilioni 1.8 kukarabati gati mojawapo katika
Bwawa la Mtera wakati bajeti ya ukarabati wa bwawa hilo ulikuwa ni Sh milioni 65.

Kamati hiyo pia imelishutumu shirika hilo kwa kushindwa kukusanya maduhuli kwani hadi kufikia Desemba mwaka 2010, Tanesco ilikuwa inawadai wateja wake Sh bilioni 245 na kati ya fedha hizo, Sh bilioni 15 zinadaiwa taasisi za serikali.

No comments:

Post a Comment