Sunday, April 29, 2012

Mkurugenzi BoT kusubiri maelezo ya kesi

Kesi yaahirishwa hadi Mei 30 mwaka huu


MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imeshindwa kumsomea maelezo ya awali Naibu Mkurugenzi wa Mifumo na Huduma wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Simon Jengo, anayetuhumiwa kwa matumizi mabaya ya ofisi kwa kununua mashine 26 za kuharibu noti kutokana na mawakili wa Takukuru kutokuwepo mahakamani.

Kesi hiyo ilikuja jana kwa ajili ya kuanza kusoma maelezo ya awalilakini Hakimu Mkazi, Ritha Tarimo aliiahirisha kwa sababu mawakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) walikuwa na udhuru.

Baada ya kutolewa kwa maelezo hayo, Hakimu Tarimo aliiahirisha hadi Mei 30 mwaka huu kwa ajili ya mshtakiwa huyo kusomewa maelezo ya awali yanayohusiana na shtaka hilo linalomkabili.
Awali, akisoma hati ya mashitaka, Mwendesha Mashitaka wa Takukuru,  Ben Lincon alidai mshtakiwa alitenda makosa hayo kati ya Januari 2005 na Desemba 2008 makao makuu ya BoT.

Alidai kuwa mshtakiwa alimshauri vibaya Gavana wa BoT katika ununuzi wa mashine 26 za kuharibu noti pasipo kujali mahitaji halisi ya benki.

Mshitakiwa yuko nje kwa dhamana ya kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika watakaosaini dhamana ya maneno ya Sh10 milioni kila mmoja.

Jengo pia anakabiliwa na kesi nyingine katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala ambapo anashtakiwa na maofisa wengine watatu wa BoT akidaiwa kughushi nyaraka kwa kampuni inayotengeneza noti za benki hiyo kwa lengo la kumdanganya mwajiri wao.

Washtakiwa wengine ni Kisima Mkango, Bosco Kimela na Ally Farjallah Bakari ambao kwa pamoja wanadaiwa kutenda makosa hayo jijini Dar es Salaam. 



Wanadaiwa kuwasilisha nyaraka kwa kampuni hiyo ili kuchapisha kiasi kikubwa cha noti tofauti na kilichoidhinishwa na mwajiri wao.

Katika mashtaka mengine wanadaiwa kuingia mkataba wa kuchapa noti kwa bei ya juu kinyume na makubaliano halali hivyo kuisababishia Serikali hasara ya Sh104,158,536,146. 


Wanadaiwa pia kuupeleka mkataba huo kwa mamlaka zinazotengeneza noti ukionyesha gharama za uongo

No comments:

Post a Comment