Sunday, April 22, 2012

Bunge lakamilisha kusikiliza mashauri ya Masaburi, Mdee

MALALAMIKO ya aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM, Philip Mangula dhidi ya Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema) na shauri linalomhusu Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Didas Masaburi anayetuhumiwa kuwatukana wabunge kuwa wanafikiri kwa kutumia makalio, yamemalizika kusikilizwa na Kamati ya Bunge.

Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge katika taarifa yake ya utekelezaji kwa mwaka 2011/12 iliyowekwa mezani mwishoni mwa wiki katika Mkutano wa Saba wa Bunge unaoendelea mjini hapa, inaeleza kuwa kamati imemaliza kusikiliza mashauri hayo na uamuzi wameupeleka kwa Spika Anne Makinda.

Mangula anamlalamikia Mdee kuwa wakati akiwasilisha hotuba ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani kwenye bajeti ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi katika mwaka huu wa fedha, alitoa kauli iliyomhusisha kuwa anamiliki hekta 2,000 za ardhi katika Kijiji cha
Wami-Dakawa wilayani Mvomero.

Baada ya kauli hiyo, Mangula aliibuka kwenye vyombo vya habari na kukanusha madai hayo ya Mdee na akamtaka athibitishe kauli yake.

Suala hilo liliwasilishwa mbele ya kamati kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge ambayo inatoa haki ya raia kujitetea na kusafisha dhidi ya kauli zinazotolewa bungeni.

“Kamati ilishughulikia suala hili hatua zake zote na taarifa ya kamati ikawasilishwa kwa spika kwa hatua zaidi,” ilieleza.

Kuhusu suala la Masaburi, liliwasilishwa baada ya Mbunge wa Kinondoni, Idd Azzan kuomba mwongozo wa Spika kuhusu kauli ya Meya huyo wa Dar es Salaam inayowadhalilisha wabunge na Spika akaamua kuamuru suala hilo lishughulikiwe na Kamati hiyo.

Taarifa hiyo iliyotiwa saini na mwenyekiti wake Hassan Ngwilizi, pia ilieleza suala hilo limemalizika kusikilizwa. Shauri la tatu ambalo lilifikishwa mbele ya kamati hiyo lilifikishwa na
Masaburi mwenyewe dhidi ya kauli zilizotolewa bungeni dhidi yake na baadhi ya wabunge.

Wabunge hao ni Godfrey Zambi ambaye ni Mbunge wa Mbozi Mashariki (CCM), Mdee na
Mbunge wa Mafia, Abdulkarim Shah (CCM).

Masaburi alilalamikia kauli za wabunge hao walizozitoa wakati wakichangia hotuba ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka huu wa fedha ambapo walimhusisha na uuzwaji wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA).

No comments:

Post a Comment