Wednesday, March 28, 2012

MATOKEO YA UCHAGUZI WILAYA YA BABATI YATENGULIWA RASMI NA TFF



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU UCHAGUZI
WA VIONGOZI WA CHAMA CHA MPIRA WA MIGUU WILAYA YA BABATI
TAREHE 27/03/2012
1. Kamati ya Uchaguzi ya TFF katika kikao chake kilichofanyika tarehe 25 Machi 2012 ilijadili mkanganyiko na mgogoro uliopo wilayani Babati kuhusu uchaguzi wa viongozi wa chama cha mpira wa Miguu Wilaya ya Babati (BDFA).

2. Kamati ilibaini kuwa mgogoro uliojitokeza kuhusu uchaguzi wa BDFA umesababishwa na Kamati ya Uchaguzi ya Mkoa wa Manyara kwa kutotimiza wajibu wake wa kusimamia uchaguzi wa BDFA na mgogoro wa uongozi ndani ya BDFA uliosababisha kuundwa kwa Kamati mbili za uchaguzi kinyume na matakwa ya Katiba ya BDFA na Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF. Kamati ya Uchaguzi ya TFF imebaini na kujiridhisha pia kuwa, mgogoro kuhusu uchaguzi wa viongozi wa BDFA umepanuka zaidi kutokana na uongozi wa BDFA kutotekeleza maagizo ya Kamati ya Uchaguzi ya TFF yaliyotolewa kwa BDFA na pia Kamati ya Uchaguzi ya MRFA kukaidi maagizo ya Kamati ya Uchaguzi ya TFF iliyoitaka Kamati ya Uchaguzi ya MRFA kusimamisha chaguzi zote Mkoani Manyara ili kuyapatia ufumbuzi mataizo ya uchaguzi yaliyojitokeza Mkoani Manyara.

3. Kwa kuwa Kamati ya Uchaguzi ya MRFA imekaidi kutekeleza maagizo ya TFF kama inavyotakiwa kwa mujibu wa Katiba ya TFF na Katiba ya MRFA na pia kwa kutotimiza kwa makusudi wajibu wake wa kusimamia kwa weledi chaguzi za wanachama wa MRFA na kuzingatia Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF, Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa mamlaka yake yaliyoainishwa katika Katiba ya TFF Ibara ya 49(1), Kanuni za Uchaguzi za TFF Ibara ya ya 6, Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF Ibara ya 10(6), 26(2) na 26(3) imeamua yafuatayo:

(i) Imefuta na kutengua matokeo ya chaguzi za viongozi wa BDFA zilizofanyika tarehe 19 Februari 2012 na tarehe 11 Machi 2012.
(ii) Imezifuta Kamati za Uchaguzi za BDFA.
(iii) Imeifuta Kamati ya Uchaguzi ya MRFA.

4. Kutokana na maamuzi hayo, TFF inaiagiza Kamati ya Utendaji ya MRFA kuchagua Kamati mpya ya Uchaguzi ya MRFA itakayozingatia matakwa ya Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF katika kutekeleza majukumu yake. Uongozi wa MRFA unatakiwa kuhakikisha kuwa Kamati ya Utendaji ya BDFA inateua Kamati mpya ya uchaguzi kwa mujibu wa Katiba ya BDFA na Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF katika Kipindi cha mwezi mmoja kuanzia tarehe ya barua hii, ili kuanza mchakato wa uchaguzi wa viongozi wa BDFA chini ya usimamizi wa Kamati ya Uchaguzi ya MRFA.

Hamidu Mbwezeleni
MAKAMU MWENYEKITI
KAMATI YA UCHAGUZI -TFF

No comments:

Post a Comment