MATOKEO YA UCHAGUZI WILAYA YA BABATI YATENGULIWA RASMI NA TFF
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU UCHAGUZI
WA VIONGOZI WA CHAMA CHA MPIRA WA MIGUU WILAYA YA BABATI
TAREHE 27/03/2012
1. Kamati ya Uchaguzi ya TFF katika kikao chake
kilichofanyika tarehe 25 Machi 2012 ilijadili mkanganyiko na mgogoro
uliopo wilayani Babati kuhusu uchaguzi wa viongozi wa chama cha mpira wa
Miguu Wilaya ya Babati (BDFA).
2. Kamati
ilibaini kuwa mgogoro uliojitokeza kuhusu uchaguzi wa BDFA umesababishwa
na Kamati ya Uchaguzi ya Mkoa wa Manyara kwa kutotimiza wajibu wake wa
kusimamia uchaguzi wa BDFA na mgogoro wa uongozi ndani ya BDFA
uliosababisha kuundwa kwa Kamati mbili za uchaguzi kinyume na matakwa ya
Katiba ya BDFA na Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF. Kamati ya
Uchaguzi ya TFF imebaini na kujiridhisha pia kuwa, mgogoro kuhusu
uchaguzi wa viongozi wa BDFA umepanuka zaidi kutokana na uongozi wa BDFA
kutotekeleza maagizo ya Kamati ya Uchaguzi ya TFF yaliyotolewa kwa BDFA
na pia Kamati ya Uchaguzi ya MRFA kukaidi maagizo ya Kamati ya
Uchaguzi ya TFF iliyoitaka Kamati ya Uchaguzi ya MRFA kusimamisha
chaguzi zote Mkoani Manyara ili kuyapatia ufumbuzi mataizo ya uchaguzi
yaliyojitokeza Mkoani Manyara.
3. Kwa kuwa
Kamati ya Uchaguzi ya MRFA imekaidi kutekeleza maagizo ya TFF kama
inavyotakiwa kwa mujibu wa Katiba ya TFF na Katiba ya MRFA na pia kwa
kutotimiza kwa makusudi wajibu wake wa kusimamia kwa weledi chaguzi za
wanachama wa MRFA na kuzingatia Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF,
Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa mamlaka yake yaliyoainishwa katika Katiba
ya TFF Ibara ya 49(1), Kanuni za Uchaguzi za TFF Ibara ya ya 6, Kanuni
za Uchaguzi za wanachama wa TFF Ibara ya 10(6), 26(2) na 26(3) imeamua
yafuatayo:
(i) Imefuta na kutengua matokeo ya chaguzi za
viongozi wa BDFA zilizofanyika tarehe 19 Februari 2012 na tarehe 11
Machi 2012.
(ii) Imezifuta Kamati za Uchaguzi za BDFA.
(iii) Imeifuta Kamati ya Uchaguzi ya MRFA.
4. Kutokana na maamuzi hayo, TFF inaiagiza Kamati ya
Utendaji ya MRFA kuchagua Kamati mpya ya Uchaguzi ya MRFA
itakayozingatia matakwa ya Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi za
wanachama wa TFF katika kutekeleza majukumu yake. Uongozi wa MRFA
unatakiwa kuhakikisha kuwa Kamati ya Utendaji ya BDFA inateua Kamati
mpya ya uchaguzi kwa mujibu wa Katiba ya BDFA na Kanuni za Uchaguzi za
wanachama wa TFF katika Kipindi cha mwezi mmoja kuanzia tarehe ya barua
hii, ili kuanza mchakato wa uchaguzi wa viongozi wa BDFA chini ya
usimamizi wa Kamati ya Uchaguzi ya MRFA.
Hamidu Mbwezeleni
MAKAMU MWENYEKITI
KAMATI YA UCHAGUZI -TFF
No comments:
Post a Comment